Вход на сайт

Просмотр новости

Найдите то, что Вас интересует

Sababu Tanzania kutunga sera mpya ya sayansi, teknolojia na ubunifu

Дата публикации: 10-08-2026 16:35:04

Serikali imeanza maandalizi ya kufanya moja ya mageuzi makubwa zaidi katika sekta ya sayansi, teknolojia na ubunifu, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuiwezesha Tanzania kujenga uchumi unaotegemea maarifa, utafiti na teknolojia za kisasa katika kipindi cha miaka 25 ijayo.

Основное содержимое страницы с новостью.

Jumanne, Agosti 11, 2026

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda

By  Jacob Mosenda

Senior Journalist with The Citizen

Mwananchi Communications Limitted

Muktasari:
  • Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuiwezesha Tanzania kujenga uchumi unaotegemea maarifa, utafiti na teknolojia za kisasa katika kipindi cha miaka 25 ijayo. 

Dar es Salaam. Serikali imeanza maandalizi ya kufanya moja ya mageuzi makubwa zaidi katika sekta ya sayansi, teknolojia na ubunifu, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuiwezesha Tanzania kujenga uchumi unaotegemea maarifa, utafiti na teknolojia za kisasa katika kipindi cha miaka 25 ijayo.

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetangaza kuwa itafanya mapitio makubwa ya Sera ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia, huku ikifikiria uwezekano wa kuandaa sera mpya kabisa itakayojulikana kama Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, ili kuendana na mabadiliko makubwa yanayoendelea duniani.

Hatua hiyo inalenga kujenga mfumo imara wa kitaasisi utakaounga mkono mnyororo mzima wa ubunifu kuanzia kwa watafiti, vyuo vikuu, wabunifu, wajasiriamali, viwanda hadi kampuni changa za teknolojia, badala ya kuendelea kuwalenga wabunifu binafsi pekee.

Akizungumza Julai 30, 2026, wakati akitangaza maandalizi ya Wiki ya Taifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu ya mwaka 2026, itakayofanyika katika Shule ya Sekondari Usagara, mkoani Tanga, kuanzia Agosti 15 hadi 24, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema mageuzi hayo ni sehemu ya maandalizi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Alisema Serikali inalenga kuhakikisha sayansi, teknolojia za kidijitali na ubunifu vinakuwa mhimili mkuu wa kukuza uchumi, kuongeza ajira, kuinua uzalishaji viwandani na kuimarisha ushindani wa Tanzania katika soko la kimataifa.

"Tunafanya mapitio ya Sera ya Sayansi na Teknolojia. Baada ya mchakato huo tunaweza kupendekeza maboresho makubwa au hata kuandaa sera mpya kabisa itakayojulikana kama Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu," alisema Profesa Mkenda.

Alifafanua kuwa lengo ni kujenga mfumo wa kitaasisi unaoweza kuendeleza mnyororo mzima wa ubunifu, kuanzia hatua ya kuzalisha wazo, kufanya utafiti, kuendeleza teknolojia hadi kufikisha bidhaa sokoni.

"Hatulengi kuwasaidia wabunifu mmoja mmoja pekee, bali tunataka kuimarisha mfumo mzima wa ubunifu,  ili mawazo yaweze kukua na kuwa bidhaa na biashara zinazoleta manufaa kwa Taifa," alisisitiza.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Profesa Carolyne Nombo, alisema sera iliyopo iliandaliwa katika mazingira tofauti na ya sasa, hivyo kuna haja ya kuifanyia maboresho makubwa ili iendane na kasi ya maendeleo ya teknolojia duniani.

"Ni muhimu sera yetu iakisi mazingira ya sasa ya dunia. Wizara inaanza mchakato rasmi wa Serikali wa kuifanyia marekebisho ili iwe mwongozo madhubuti wa maendeleo ya sayansi, teknolojia na ubunifu nchini," alisema.

Ni wakati mwafaka

Mapitio hayo yanafanyika wakati mataifa mengi barani Afrika yanaongeza uwekezaji katika teknolojia ya akili unde (AI), uchumi wa kidijitali, teknolojia za kisasa za uzalishaji, bioteknolojia na biashara zinazotokana na matokeo ya utafiti wa kisayansi kama sehemu ya mkakati wa kukuza uchumi.

Sambamba na mageuzi hayo ya sera, Serikali imewataka Watanzania kuendelea kutumia bidhaa na teknolojia zinazobuniwa nchini, ili kuongeza soko la ndani kwa wabunifu wazawa na kuchochea ukuaji wa sekta ya ubunifu.

Maofisa wa wizara walisema tayari miongozo imeandaliwa ili kuhakikisha bidhaa na huduma zinazotokana na ubunifu wa ndani, zinapewa kipaumbele, hatua itakayowasaidia wabunifu kubadilisha matokeo ya kazi zao za kitafiti kuwa biashara zenye tija.

Wakati huo huo, Mkurugenzi wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu katika wizara hiyo, Profesa Ladislaus Mnyone, alisema Serikali imeidhinisha mkakati wa kuongeza ushiriki wa Watanzania wanaoishi nje ya nchi katika kutambua fursa zinazoweza kusaidia maendeleo ya ubunifu nchini.

Alisema pia Serikali imepanua mfumo wa kutambua wabunifu, ambapo sasa hautategemea tena mashindano ya kitaifa ya Makisatu pekee, bali utatumia mifumo mingine ya kubaini bunifu zenye uwezo wa kuleta mabadiliko.

"Hadi sasa, halmashauri 90 nchini zimeanzisha madawati ya sayansi, teknolojia na ubunifu yatakayowawezesha wabunifu kupata ushauri, kuunganishwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech) pamoja na wadau wengine kwa ajili ya kupata msaada wa kitaalamu na kifedha," alisema Profesa Mnyone.

Kupitia madawati hayo, wabunifu watapata fursa ya kupata ushauri, mafunzo, mitandao ya kitaalamu na msaada wa Serikali utakaowawezesha kupeleka mawazo yao kutoka maabara na karakana hadi sokoni.

Profesa  Mkenda alisema Wiki ya Taifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu ya mwaka huu itawakutanisha wadau mbalimbali, kutoka wizara, vyuo vikuu, vyuo vya ufundi, vyuo vya ualimu, taasisi za utafiti, kampuni za teknolojia, wabunifu, washirika wa maendeleo, shule za msingi na sekondari pamoja na sekta binafsi.

Alisema kongamano hilo litatoa fursa ya kuonesha teknolojia mpya, kubadilishana uzoefu na kujadili mikakati ya kuimarisha elimu, maendeleo ya ujuzi na ubunifu kwa kuzingatia vipaumbele vya taifa.

Wiki hiyo pia itahusisha Mashindano ya Kitaifa ya Ubunifu ya Makisatu, yanayofanyika kila mwaka tangu 2019. Mashindano hayo yamezalisha bunifu mbalimbali zilizofanikiwa kuingia sokoni, zikiwemo mashine za kukamua mafuta ya parachichi, mabegi ya shule yanayotumia nishati ya jua, viti mwendo kwa watu wenye ulemavu na mita za maji za kisasa.

Wataalamu wa elimu wanaamini kuwa kuimarisha sayansi, teknolojia na ubunifu kutakuwa msingi muhimu wa kuiwezesha Tanzania kupata rasilimali watu yenye ujuzi unaohitajika katika uchumi wa viwanda, kupanua uzalishaji wenye thamani kubwa na kushindana katika uchumi wa kidijitali unaozidi kukua duniani.

Схожие новости

#Наименование новостиТональностьИнформативностьДата публикации
1Правительство прорабатывает восемь проектов по формированию высокотехнологичной экономики0003-03-2021
2Чернышенко: Россия ставит цель увеличить в 2,5 раза затраты на исследования к 2030 году0017-02-2022
3Mafundisho ya dini yanavyosahaulika katika malezi ya watoto05.6209-08-2026
4Правительство предлагает ускорить технологическое развитие экономики0002-06-2020
5Правительство планирует повысить в два раза спрос на российские IT-сервисы0022-07-2020
6Правительство одобрило законопроект о формировании единой системы поддержки инноваций0004-07-2020
7Кабмин увеличит финансирование научных исследований в образовательных учреждениях0008-02-2021
8Власти Татарстана разработают мобильную платформу с сервисами для молодежи0030-01-2019
9Минвостокразвития предлагает расширить налоговые льготы для высокотехнологичных проектов0031-07-2020
10Mafanikio darasani yanaanzia kwenye afya ya mwili07.8310-08-2026

Классификация: Национальные проекты. Схожих патентов: 0. Схожих новостей: 10. Тональность: 0. Информативность: 7.3. Источник: www.mwananchi.co.tz.